JKT KUENDELEA KUUNGA MKONO JUHUDI ZA SERIKALI KUTATUA CHANGAMOTO ZA UPATIKANAJI WA MAFUTA YA KULA NCHINI
Mkurugezi Mtendaji wa Shirika la Uzalishaji Mali la Jeshi la Kujenga Taifa( SUMAJKT), Kanali Petro Ngata amesema Jeshi la Kujenga Taifa litaendelea kuunga mkono juhudi za Serikali katika kutatua changamoto ya upatikanaji wa mafuta ya kula hapa nchini.
Ameyasema hayo wakati alipotembelea Banda la JKT katika Maonesho ya Waku- lima,Wafugaji na Wavuvi (Nanenane) yanayofanyika Kitaifa katika viwanja vya John Mwakangale, Uyole Jijini Mbeya.
Kanali Ngata amefafanua kuwa, JKT limeanza kutekeleza Kilimo cha Mazao ya Kimkakati ikiwemo zao la Alizeti kwa kutumia mashamba yake makubwa katika maeneo ambayo zao hilo linastawi.
"Tumeanza na Mkakati wa Kulima kwa wingi mazao ya kimkakati, na hatua inayofuata ni kuchakata zao hilo na kupata mafuta ya Kula". Amesema Kanali Ngata
Akizungumzia namna JKT mashamba darasa ya JKT yalivyo na Manufaa, Kanali Ngata amesema JKT lina wataalamu wa kutosha waliobobea katika kutoa elimu bora ya Uzalishaji wa Mazao ya kilimo, Mifugo na Uvuvi hivyo amewataka wakazi wa Mbeya na Mikoa ya Jirani kutembelea Banda la JKT.
Nae Mwenyekiti wa Maonesho ya Nanenane Kanali Shija Lupi amewataka
wananchi kujitokeza kwa wingi kutembelea Banda la JKT kwa lengo la kupata elimu sambamba na kujionea shughuli mbalimbali zinazofanywa na JKT pamoja na Bidhaa zinazozalishwa na Viwanda na Makampuni Tanzu ya SUMAJKT.
Sambamba na hilo, Kanali Lupi amesema Maonesho ya mwaka huu yana kauli mbiu inayoendana na Ajenda ya Kitaifa ya Sensa ya watu na Makazi hivyo amewataka wananchi kujitokeza katika zoezi la sensa kwa maendeleo ya Taifa hili.
Akitoa ufafanua wa namna ya kufanya uvuvi wenye tija, Mkurugenzi wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi Kanali Peter Lushika amesema uvuvi kwa njia ya mabwawa ni sahihi kwa Jiji la Mbeya kwa sababu samaki hawahitaji baridi kali, hivyo uvuvi jwa njia ya matanki unaweza kupelekea samaki wakafa.
Maonesho ya Wakulima (Nanenane) yanaadhimishwa kila tarehe 8 ya Mwezi Agosti kwa kila mwaka nchini, lengo likiwa kutoa Elimu kwa wakulima, Wafugaji na Wavuvi ya njia bora za Uzalishaji wenye Tija.
Jeshi la Kujenga Taifa, Linashiriki maonesho hayo Kitaifa na kikanda kwa lengo la kuwafikia wananchi wa Tanzania nchi nzima ambayo ni zaidi ya asilimia 80 wanaujihusisha na kilimo, Mifugo na Uvuvi.
Comments
Post a Comment