Shirika la Uzalishaji Mali la Jeshi la Kujenga Taifa (SUMAJKT) kupitia Kampuni tanzu iitwayo SUMAJKT shoes and leather Products Co LTD. tarehe 04 Novemba 2022 limekabidhi viatu vya ngozi jozi 500 kwa Taasisi ya Mama Ongea na Mwanao yenye kauli mbiu “Samia nivike viatu”.
Aidha, makabidhiano ya viatu hivyo yamefanyika Makao Makuu ya SUMAJKT Mlalakuwa Dar es salaam.
Akielezea historia ya kiwanda Mkurugenzi Mwendeshaji wa kiwanda hicho Meja Mathias John amesema, Kiwanda cha viatu na bidhaa za ngozi SUMAJKT Shoes and Leather Product Co. LTD Kilianzishwa Jul 2017 na majukumu yake yakiwa ni uzalishaji wa viatu na bidhaa mbalimbali za ngozi.
Aidha, toka kuanzishwa Kqa kiwanda hicho kimeendelea kuongeza uwezo wa uzalishaji kwa kununua vifaa na mashine za kisasa ili kuzalisha bidhaa zenye ubora.
Bidhaa zinazozalishwa ni viatu kwa ajili ya taasisi za ulinzi, viatu vya usalama (safety boots), viatu vya maofisini na viatu vya shule.
Uwezo wa kiwanda ni kuzalisha viatu jozi 500 kwa siku na Kupitia uzalishaji wa bidhaa hizo kiwanda kimeweza kuzalisha viatu kwa ajili ya watoto wa kitanzania walio shule za msingi kupitia Kampeni ya Mama ongea na mwanao 2021 yenye kauli mbiu Samia nivishe viatu.
Aidha, Mkurugenzi Mwendeshaji wa kiwanda hicho Meja Mathias John mara baada ya historia hiyo fupi, amekabidhi jozi 500 za viatu kwa kamati inayosimamia kampeni hiyo kwa ajili ya kuwavisha wanafunzi wa shule mbalimbali za msingi.
“Nichukue fursa hii kuwakaribisha SUMAJKT kwani ni kituo cha huduma na bidhaa bora,
SUMAJKT Shoes and Leather Product Company Limited, Tunakabidhi viatu hivi kwa taasisi ya mama ongea na mwanao na lengo ni kuunga mkono juhudi zinazofanywa na Taasisi hii.
SUMAJKT tukiwa sehemu ya wazazi na walezi kwa watoto, tumeona jambo hili lililobebwa na taasisi hii ni jema na ni la jamii nzima na tumeguswa kuwainua watoto hasa wa vijijini ili wasome kwa utulivu .
Tunaipongeza Taasisi hii ya mama ongea na mwanao kwa kuleta tabasamu kwa watoto wa kusini na kuitakia kampeni hii mafanikio makubwa. ” alisema Maj John
Nae Mwenyekiti wa Taasisi ya Mama ongea na mwanao ndg. Steven Nyerere kwa niaba ya kamati hiyo alishukuru SUMAJKT kuunga mkono kampeni yao yenye nia ya kuwavisha viatu watoto vijijini.
“Tunaishukuru SUMAJKT kwa kuunga mkono jambo letu na leo tunaweka bondi na Shirika hili . Viatu hivi hatuendi kuwakabidhi wakuu wa shule, tutawavalisha watoto sisi wenyewe na tunawakaribisha wadau mbali mbali kutuunga mkono na itapendeza kama viatu vikinunuliwa katika kiwanda cha SUMAJKT kwa sababu ni viatu vya kudumu ambavyo mtoto anaweza kuvaa hadi miaka miwili “ alisema.
Kiwanda cha viatu na bidhaa za ngozi SUMAJKT kimekuwa kikitengeneza viatu na bidhaa za ngozi halisi vya aina mbali mbali kwa matumizi ya watu wa rika tofauti.
Comments
Post a Comment