Mkuu wa Wilaya ya Tunduru Mhe. Julius Mtatiro, ameahidi kuongeza mikakati ya uwekezaji katika shamba la kilimo cha korosho na ufugaji wa ng'ombe,
mbuzi na kuku linalomikiwa na Shirika la Uzalishaji
Mali la Jeshi la Kujenga Taifa (SUMAJKT) katika Wilaya ya Tunduru.
Mhe. Mtatiro, amezungumza hayo leo tarehe 22 Julai 2022, alipokuwa akizindua shamba hilo lililopo katika kijiji cha Nanjoka, Wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma.
Katika uzinduzi huo Mhe. Julius Mtatiro, ametoa pongezi kwa Mkuu wa Jeshi la Kujenga Taifa na Afisa Mtendaji Mkuu wa SUMAJKT Meja Jenerali Rajabu Nduku Mabele na pia kwa Mkurugenzi Mtendaji wa SUMAJKT Kanali Petro Ngata kwa kazi kubwa
ambayo wamedhamiria kwenye wilaya ya Tunduru.
"Naishukuru SUMAJKT kwa kulichagua eneo hili kuendesha shughuli za kilimo pamoja ufugaji, ambazo zitakuza uchumi na kuzalisha ajira kwa wingi katika maeneo yetu mbalimbali ", alisema Mhe. Mtatiro.
Mhe. Julius Mtatiro, amemtaka Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Tunduru Bw. Chiza Marando, aendelee kukaa na wataalamu kuangalia maeneo ya mkakati yaliyotengwa kwa ajili ya kilimo cha "Block Farming" ili wapewe SUMAJKT.
Nae Kaimu Mkurugenzi wa Viwanda SUMAJKT Meja Peter Kulyakwave, akimwakilisha Mkurugenzi Mtendaji wa SUMAJKT Kanali Petro Ngata, katika uzinduzi wa shamba hilo ameeleza kuwa Shirika linatekeleza mkakati wake wa kuongeza vyanzo vipya vya mapato na kuboresha huduma mbalimbali zikiwemo kilimo cha korosho, ufugaji wa ng'ombe kwa ajili ya kuwanenepesha na kuuza, mbuzi pamoja na kuku.
Kwa upande wa Mkurugenzi Mwendeshaji wa SUMAJKT Port and Services Co. Limited, Meja Joseph Marwa, ameeleza kuwa Kampuni hiyo ilikabidhiwa shamba hilo la korosho lenye ukubwa wa hekari 2180 na Shirika la Uzalishaji Mali Ia Kujenga Taifa mnamo mwaka 2017 na
iliweka mipango ya kuelendeleza shamba hilo kwa awamu, ambapo walianza kupanda mikorosho mipya idadi 3000, lengo likiwa kuendeleza kupanda mikorosho mipya kufikia hekari 600.
Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) kupitia SUMAJKT lilianza kukalia eneo hilo mwaka 2019, ambapo Kampuni ya SUMAJKT Port and Services Co. Ltd. Ilikabidhiwa kuendesha shamba hilo.
Comments
Post a Comment