Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ameaga kaya zingine 25, zenye watu 105, na amesema mpaka kufikia tarehe 18/8/2022, jumla ya kaya 1,002 zenye watu 5,382 zimejiandikisha kwa hiari kuhama katika eneo la hifadhi ya Ngorongoro na kuelekea kijiji cha Msomera wilayani Handeni mkoa wa Tanga, lililotengwa na serikali kwa ajili ya wakazi hao.
Kati ya kaya hizo, tayari kaya 624 zenye watu 3,323 zimehakikiwa na kufanyiwa uthamini na kati ya kaya hizo, kaya 106 zenye watu 536 zimeshahamia kijiji cha Msomera wilayani Handeni Mkoani Tanga.
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amesema hayo Agosti 19,2022 Mkoani Arusha sambamba na zoezi la kukabidhi hundi ya Malipo kwa wakazi wapya wa Msomera. Hafla fupi ilifanyika kwenye ofisi za mamlaka ya hifadhi hiyo kwa nia ya kufanikisha hatua hiyo.
Aidha , Mhe. Kassim Majaliwa ameeleza kuwa, Rais Samia Suluhu Hassan amepongeza uamuzi wa wananchi hao na kwamba serikali itaendelea kuwekeza katika kuboresha miundombinu ya eneo la Msomera.
“Napenda kumhakikishia Mheshimiwa Rais kwamba tulianza kuratibu, tunaendelea kuratibu na kuhakikisha wote walioamua kuhama wanapata faraja.” amesema Waziri Mkuu
Amesema zoezi la kuratibu uhamaji wa hiari kuelekea Msomera limefanywa kwa utaratibu mzuri ikiwa ni pamoja na kuzingatia mazingira rafiki yaliyoko katika eneo la Msomera kwa binadamu na mifugo ambayo ni miundombinu ya barabara, umeme, maji, shule huduma za afya na huduma nyingine za kijamii ikiwemo uwezo wa umiliki wa ardhi, kilimo na malisho.
Shirika la Uzalishaji Mali la Jeshi la Kujenga Taifa SUMAJKT kupitia kampuni yake ya ujenzi SUMAJKT Construction Company Limited, ilipewa jukumu la kujenga nyumba 402 za kuhamia wakazi hao ambapo kampuni hiyo inaendelea na ujenzi huo kwa kasi na inatarajia kukabidhi nyumba hizo kwa serikali ifikapo Septemba 30, 2022.
Comments
Post a Comment