MAMLAKA YA MAPATO TANZANIA (TRA) KUTOA MILIONI ISHIRINI NA TISA KUKARABATI MADARASA JITEGEMEE SEKONDARI
Kamishina Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ndugu Alphayo Kidato ameahidi kutoa kiasi cha milioni ishirini na tisa za kitanzania kwa ajili yakukarabati Madarasa pamoja na Mabweni ya wanafunzi wa shule ya Sekondari ya Jitegemee JKT iliyopo Wilaya ya Temeke Jijini Dar es salaam.
Ahadi hiyo imetolewa leo tarehe 29 Octoba 2022 na Mkurugenzi wa huduma na elimu kwa mlipa kodi Mamlaka ya Mapato Tanzania ndugu Richard Kayombo kwa niaba ya Kamishina Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania ndugu Alphayo Kidato aliyemwakilisha katika mahafali hayo ya 38 ya kidato cha nne 2022.
Kayombo alitoa shukrani za pongezi kwa uongozi wa shule ya Jitegemee kwa kuona umuhimu wa Kamishina Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kuwa sehemu ya familia ya Jitegemee katika mahafali ya 38 ya wanafunzi wa kidato cha nne.
Pia Mkurugenzi wa huduma na elimu kwa mlipa kodi Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ndugu Richard Kayombo amewasihi wahitimu na wanafunzi wengine kuhakikisha wanaongeza nidhamu katika masomo ili waweze kufanya vizuri katika mitihani yao.
Nae mwenyekiti wa Bodi ya shule ya Sekondari Jitegemee Brigedia Jenerali (Mstaafu) Laurance Magere ametoa pongezi nyingi kwa Mkurugenzi wa huduma na elimu kwa mlipa kodi ndugu Richard Kayombo kwa niaba ya Kamishina Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ndugu Alphayo Kidato kwa mchango wao mkubwa walioahidi kwa ajili ya kukarabati miundombinu ya madarasa na Mabweni ili kuhakikisha shule inakuwa na muonekano mpya na wa kisasa.
Kwa upande wa mkuu wa Shule ya Sekondari ya Jitegemee Kanali Robert kessy amesema wataendelea kuwatumia wadau mbalimbali katika harakati za ukarabati wa miundombinu ya Shule, huku akimpongeza Mkurugenzi wa huduma na elimu kwa mlipa kodi ndugu Richard Kayombo kwa niaba ya Kamishina Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ndugu Alphayo Kidato pamoja na wazazi kwa kuwa sehemu ya mahafali ya 38 ya wanafunzi wa kidato cha nne.
Pia Kanali Robert kessy ametoa shukrani za dhati kwa walimu na watumishi wengine wa Shule ya Jitegemee kwa namna wanavyojitoa kuhakikisha wanafunzi wanajifunza na kufanya vizuri ikizingatiwa kwamba shule ya Sekondari Jitegemee inachukua wanafunzi wenye ufaulu wa kawaida kulinganisha na shule zingine nchini.
Mahafali hayo ya kidato cha nne ni ya 38 tangu kuanzishwa kwa shule ya Jitegemee inayomilikiwa kwa sasa na shirika la Uzalishaji Mali la Jeshi la Kujenga Taifa (SUMAJKT), huku idadi ya wanafunzi 132, wavulana idadi 81 na wasichana idadi 51, wakitarajia kufanya mitihani yao ya mwisho tarehe 14 Novemba 2022 na kuhitimu rasmi elimu ya kidato cha nne.
Mgeni rasmi katika mahafali hayo ndugu Richard Kayombo, Mkurugenzi wa huduma na elimu kwa mlipa kodi Mamlaka ya Mapato Tanzania, kwa niaba ya Kamishina Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ndugu Alphayo Kidato, aliwasili shuleni na kupokelewa na Mkuu wa shule ya Sekondari Jitegemee Kanali Robert kessy na kumpatia taarifa fupi ya maendeleo ya Shule, na kumuomba kuwashika mkono katika harakati za kukarabati miundombinu ya madarasa na Mabweni ya wanafunzi kabla ya kumtembeza kuangalia baadhi ya majengo hayo.
Mwisho wanafunzi wa kidato cha nne wanaotarajia kufanya mitihani yao ya mwisho tarehe 14 Novemba 2022 wamefurahishwa na mgeni rasmi wa mahafali yao kutoa ahadi ya kiasi cha milioni 29 za kitanzania kukarabati miundombinu ya madarasa nMabweni ya wanafunzi, huku wakisema mchango huo utachochea zaidi wanafunzi kujituma katika masomo na kufanya vizuri katika mitihani yao.
Comments
Post a Comment